RAIS MAGUFULI ATEMBELEA WAGONJWA HOSPITALI YA TAIOFA MUHIMBILI WAKWEMO KINGUNGE NA MAPACHA WALIOUNGANA

Mapacha walioungana
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli leo amewajulia hali baadhi ya wagonjwa waliolazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete Jijini Dar es Salaam wakiwemo Mzee Kingunge Ngombale Mwiru na Mapacha walioungana Maria na Consolata Mwakikuti.
Katika wodi ya Mwaisela,Mhe.Rais Magufuli amemjulia hali Mzee Kingunge Ngombale Mwiru ambaye anatibiwa majeraha baada ya kushambuliwa na mbwa wake nyumbani kwake Jijini Dar es Salaam.
Kingunge Mwiru
Dkt.Ibrahim Mkoma wa hospitali hiyo amemueleza Mhe.Rais Magufuli kuwa hali ya Mzee Kingunge inaendelea vizuri ambapo Mzee Kingunge amemshukuru Mhe.Rais Magufuli kwa kumwona hospitalini hapo na amemueleza kuwa sasa anajisikia nafuu baada ya kupata matibabu.
Pamoja na kumpa pole na kumuombea apone haraka,Mhe.Rais Magufuli amesema anatambua mchango mkubwa wa Mzee Kingunge katika siasa na maendeleo ya nchi.
Rais pia Katika wodi ya Sewahaji,amemjulia hali Bw.Richard Kajumulo ambaye ni Kaka wa Mbunge wa Muleba Kusini Prof. Anna Kajumulo Tibaijuka,Bw.Said Abeid Salim,Bi.Amina Ismail Shirwa,Mzee Hamad Lila na amempa pole Naibu Katibu Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt.Zainab Chaula aliyefiwa na Mama yake mzazi wakati Mhe.Rais akiwa wodini humo.
Wakati huo huo, Mhe.Rais Magufuli amewajulia hali mapacha walioungana Maria na Consolata Mwakikuti ambao wamelazwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete kwa matibabu ya moyo.
Maria na Consolata wamemshukuru Mhe.Rais Magufuli kwa kuwaona na kuwapa pole huku mapacha hao wakiongoza sala ya kumuombea Mhe.Rais Magufuli na nchi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete Prof.Mohamed Janabi amesema matibabu kwa Maria na Consolata ambao ni wanafunzi mwaka wa kwanza katika Chuo Kikuu cha Kanisa Katoliki Ruaha (RUCU) yanakwenda vizuri.
Aidha,Prof.Janabi amesema taasisi hiyo imefanikiwa kutoa matibabu kwa wagonjwa wa moyo 14,000 katika mwaka uliopita na kwamba inashika nafasi ya tatu barani Afrika kwa utoaji wa huduma bora za matibabu ya moyo.
Aidha Mhe.Rais Magufuli amewashukuru na kuwapongeza madaktari wa hospitali ya Taifa Muhimbili na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete kwa kazi kubwa wanayofanya kutibu wagonjwa na amesema Serikali itaendelea kutatua changamoto zinazowakabili ili kuboresha huduma zaidi.

Habari zaidi ni P5TANZANIA LIMITED

Comments

Popular posts from this blog

HISTORIA FUPI YA ABDULRAHMAN KINANA ALIYEJUZULU UKATIBU MKUU CCM

FAHAMU HISTORIA YA JOKETI ALIYETUMBULIWA NA UVCCM

HISTORIA FUPI YA LAZARO NYALANDU ALIYEIBWAGA CCM NA KUHAMIA CHADEMA