WIZARA YA AFYA ZANZIBAR KUSHIRIKIANA NA MSD KATIKA UAGIZAJI DAWA NA VIFAA TIBA


WIZARA  ya Afya Zanzibar imetiliana saini makubaliano ya ushirikiano na Bohari ya Dawa Tanzania (msd) katika masuala ya uagiziaji dawa na vifaa Tiba kutoka viwandani moja kwa moja na hatua hiyo itaiwezesha Zanzibar kupunguza gharama kubwa ya kuagiza dawa kutoka katika makampuni.
Katibu Mkuu Wizara ya Afya Bi. Asha Abdalla Juma alitia saini kwa upande wa Wizara hiyo na Mkurugenzi  Mkuu Laurean Rugambwa Bwanakunu aliiwakilisha Bohari kuu ya Dawa Tanzania katika sherehe zilizofanyika Wizara ya Afya Zanzibari Mnazimmoja.
Akizungumza baada ya kutiliana sani Bi. Asha Abdalla alisema ushirikiano huo utaisaidia Serikali na wananchi kwa ujumla kuwa na uhakika wa upatikanaji dawa na kupunguza mzigo wa kutumia gharama kubwa kuagiza dawa.
Alisema hatua hiyo ni utekelezaji wa maagizo ya Serikali kuhakikisha  dawa zote zinapatikana  bila usumbufu katika Hospitali na vituo vya afya na kufanikisha  malengo yake ya kuwapatia wananchi  huduma bora za afya.
Katibu Mkuu Wizara ya Afya ameshauri mashirikiano yaliyoanzishwa baina ya Bohari  Kuu ya Dawa Zanzibar na Bohari Kuu ya Tanzania yawe endelevu na kuwa mfano kwa Taasisi nyengine za pande mbili za Muungano na ukanda mzima wa Afrika Mashariki.
Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa Tanzania Laurean Rugambwa Bwanakunu ameihakikishia Wizara ya Afya kwamba watatoa huduma bora kwani dawa wanazoagiza ni za uhakika  na zenye ubora .
Alisema wamejipanga kikamilifu kuhakikisha wanatoa dawa na vifaa tiba na hivi sasa wameingia mikataba na viwanda vikubwa  vya kuzalisha dawa vya  ndani na nje ya Tanzania kwa ajili ya kutoa huduma bora kwa wananchi.
Amewapongeza maafisa wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  waliosimamia na kufanikisha mpango huo kwa muda mfupi bila ya kuwa na urasimu katika utekelezaji wake.
Ameishukuru Wizara ya Afya kwa kuwaamini na kukubali kushirikiana nao katika kazi ya uagizaiaji wa dawa na vifaa Tiba na amewahakikishia kwamba kazi hiyo wataifanya kwa pamoja katika viwanda vya kuzalisha dawa.
Hata hivyo Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa Tanzania amewashauri wawekezaji wa Zanzibar kuwekeza viwanda vya dawa kwa lengo la kupunguza kuagiza bidhaa hiyo kutoka viwanda vya nje.
Alisema kati ya viwanda vitano vya dawa walivyoingia mkataba wa kununua dawa hakuna hata kiwanda kimoja kutoka Zanzibar wakati wafanyabiashara wenye  uwezo wa  kuwekeza katika sekta hiyo wapo.
Habari zaidi ni P5TANZANIA LIMITED

Comments

Popular posts from this blog

HISTORIA FUPI YA ABDULRAHMAN KINANA ALIYEJUZULU UKATIBU MKUU CCM

FAHAMU HISTORIA YA JOKETI ALIYETUMBULIWA NA UVCCM

HISTORIA FUPI YA LAZARO NYALANDU ALIYEIBWAGA CCM NA KUHAMIA CHADEMA