RAILA ODINGA AJIONDOA KATIKA UCHAGUZI WA MARUDIO KENYA



Kiongozi mkuu wa upinzani nchini Kenya Raila Odinga ametangaza kuwa hatashiriki kwenye uchaguzi mkuu ambao umepangwa kufanyika tarehe 26 mwezi huu.

Bwana Odinga anasema anataka kufanyika uchaguzi mpya jinsi ilivyoamuliwa na mahakama ya juu.
Uchaguzi huo wa tarehe 26 utakuwa ni marudio ya uchaguzi mkuu, baada ya mahakama ya juu nchini Kenya kufuta matokeo ya uchaguzi wa tarehe 8 mwezi Agosti mwaka huu.
Bw. Odinga anasema amejiondoa ili kuipa tume ya uchaguzi IEBC muda wa kutosha kufanya mabadiliko ambayo yatawezesha kufanyika uchaguzi kwa njia nzuri.
Awali tume ya uchaguzi ilikuwa imemtangaza rais wa sasa Uhuru Kenyatta kuwa mshindi.Ilisema kuwa Bw. Kenyatta alishinda uchaguzi huo kwa kura milioni 1.4.
Upinzani nchini Kenya awali ulikuwa umetangaza wazi kuwa ungeshiriki kwenye uchaguzi mkuu ikiwa mabadiliko yanayostahili yangefanyika.
Upinzani unaamini kuwa uchaguzi unastahili kufutwa baada ya Odinga kujiondoa, na kutoa muda wa kutosha kufanyika mabadiliko yanayostahili ili uchaguzi kufanyika kuambatana na sheria na katiba.
Serikali imekuwa ikisema kuwa uchaguzi utafanyika na rais kuapishwa.Bw. Odinga pia ametoa wito kwa watu kuandamana  Jumatano hii kwa kutumia kauli mbiu "hakuna mabadiliko, hakuna uchaguzi".
Mwezi Septemba mwendesha mashtaka mkuu nchini Kenya Keriako Tobiko, aliamrisha polisi na tume ya kupambana na ufisadi kuchunguza ikiwa wanachama wa tume ya uchaguzi walihusika na uhalifu wowote.
Alitaka wachunguzi kuchunguza madai kuwa maafisa wawili wakuu wa upinzani walikuwa wamedukua mitandao ya tume ya uchaguzi.

Comments

Popular posts from this blog

HISTORIA FUPI YA ABDULRAHMAN KINANA ALIYEJUZULU UKATIBU MKUU CCM

FAHAMU HISTORIA YA JOKETI ALIYETUMBULIWA NA UVCCM

HISTORIA FUPI YA LAZARO NYALANDU ALIYEIBWAGA CCM NA KUHAMIA CHADEMA