WAZIRI MKUU ASEMA HANA KINYONGO NA MTU YEYOTE,ASEMA ITIKADI ZA SIASA ZILIISHIA OKTOBA 25


Na.OFISI YA WAZIRI MKUU.
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema hana kinyongo na mtu yeyote kwa sababu alitangaza msamaha siku aliyokabidhiwa cheti kuwa mbunge wa jimbo la Ruangwa na kusisitiza kuwa siasa ziliisha tangu Oktoba 25, mwaka huu.
                                      
Waziri Mkuu Kasim Majaliwa akizungumza na Wakazi Mkoani Lindi

Ametoa kauli hiyo jana jioni wakati akizungumza na mamia ya wananchi waliofika kumsikiliza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa mikutano wa Likangala wilayani Ruangwa, mkoani Lindi.
“Sina kinyongo na mtu yeyote na roho yangu iko huru, hivi ndiyo nilivyo. Nilikwishatangaza msamaha kwa hiyo ninawaomba wale niliowakwaza nao pia wanisamehe… lakini ninawasihi kuwa milango iko wazi, wawe huru kurudi wakati wowote,” alisema huku akishangiliwa na wananchi hao.
“Ninawataka twende pamoja ili tulete maendeleo ya Ruangwa, huku nikisisitiza kaulimbinu yangu ya kampeni kwamba Ruangwa kwa Maendeleo Inawezekana. Wao warudi tu, nitawahudumia wote bila kujali itikadi zao.”
Aliwaeleza wakazi hao wa Ruangwa na vitongoji vyake kwamba amekuja kuwashukuru kwa kumchagua na kumpa kura nyingi la sivyo asingefanikiwa kuwa mbunge wao. “Kikubwa ninamshukuru Mungu aliyemuongoza Mheshimiwa Rais pamoja na Makamu wake hadi wakanipa jukumu hili,” alisema.
“Kipekee ninamshukuru Mungu aliyemuongoza Mheshimiwa Rais na kutupa sisi wana Ruangwa tusaidiane kulibeba jukumu hili. Ninawahakikishia kuwa pamoja na jukumu hili la kitaifa, sitawaacha wala sitawaangusha. Nitakwenda mikoa mingine hapa nchini ili kuwasikiliza na kuwahudumia Watanzania huku nikijua kwamba mpo salama,” alisema.
Aliwaeleza wananchi hao kwamba bila kujali itikadi za vyama, ameunda timu ya madiwani 22 kutoka kata zote za jimbo hilo ambayo atafanya nayo kazi kwa karibu ili kuhakikisha matarajio ya wana-Ruangwa yanatimia. Madiwani wanane kati hao 22 wanatoka UKAWA na 14 wanatoka Chama cha Mapinduzi (CCM).
Akigusia mipango ya maendeleo kwa jimbo hilo, Waziri Mkuu alisema ameamua kuweka umeme wa nishati ya jua kwenye shule zote na zahanati zote ambazo hazitafikiwa na umeme wa gridi ya Taifa kwa sababu ziko pembezoni mwa jimbo hilo.
“Nafanya hivi kwa sababu sipendi watoto wetu wakose masomo ya jioni kwa sababu ya kukosa umeme au washindwe kufanya mafunzo kwa vitendo (practicals) kwa vile wamekosa umeme,” alisema.
Mapema, akiwa njiani kuelekea Ruangwa, Waziri Mkuu alisimama kwa muda kijijini kwao Nandagala katika kata ya Mnacho, na kuwasalimia wananchi waliojitokeza kumpokea kwa nderemo na hoihoi kibao.
Katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa kijijini hapo, Waziri Mkuu alikabidhiwa zawadi mbalimbali yakiwemo mavazi ya kimila pamoja na silaha za jadi.
Aliwataka wakazi hao wamvumilie kwa sababu ratiba sasa itabadilika na hawatamuona mara kwa mara kama ilivyokuwa awali kwa vile anapaswa awahudumie Watanzania wote. “Zile safari za jimboni zitapungua sana lakini mjue ni kwa sababu niko kwa ajili ya Watanzania wote wa nchi hii,” alisema.
“Ninaomba dua zenu ili niendelee kuwa mwadilifu na muwajibikaji,” aliwaomba na kususutiza kwamba waendelee kumuombea yeye pamoja na viongozi wengine wa kitaifa ili waweze kutimiza yale ambayo Watanzania wanatamani yatokee.

Comments

Popular posts from this blog

HISTORIA FUPI YA ABDULRAHMAN KINANA ALIYEJUZULU UKATIBU MKUU CCM

FAHAMU HISTORIA YA JOKETI ALIYETUMBULIWA NA UVCCM

HISTORIA FUPI YA LAZARO NYALANDU ALIYEIBWAGA CCM NA KUHAMIA CHADEMA