RAIS MAGUFULI ASISITIZA SERIKALI KUSHIRIKIANA NA VIONGOZI WA DINI KULETA MAENDELEO


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli amesema Serikali ya Awamu ya Tano itaendelea kushirikiana na viongozi wa dini katika masuala mbalimbali ya maendeleo hapa nchini.
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo katika Ibada ya kumsimika Mhashamu Askofu Isaac Amani kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Arusha iliyofanyika katika viwanja vya Kanisa la MtakatifuTeresia wa Mtoto Yesu Jijini Arusha.
Mhashamu Askofu Isaac Amani aliyekuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Moshi aliteuliwa na Baba Mtakatifu Francis tarehe 27 Desemba,2017 kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo hilo na amesimikwa na Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Arusha Mhashamu Josephat Louis Lebulu na Balozi wa Baba Mtakatifu hapa nchini Askofu Mkuu Marek Solczynski.
Hatua ya rais Rais Magufuli kuhudhuria ibada hii ya kanisa katoliki imechukuliwa kama ishara bora ya kurejesha uhusiano mwema na baadhi ya makanisa makuu ya kikristo likiwemo kanisa katoliki ambao wamekua wakiikosoa vikali serikali yake.
Katika hatua nyingine,Mh.Rais Magufuli amechangia mifuko 300 ya saruji kwa ajili ya ujenzi Kanisa Kuu jipya la Mtakatifu Teresia wa Mtoto Yesu ambalo ujenzi wake unaendelea.
Katika risala iliyosomwa na Padre Alois Kitomari kwa niaba ya familia ya Mungu Jimbo Kuu Katoliki la Arusha, imempongeza rais Magufuli kwa juhudi zake za kusimamia vizuri nidhamu ya utumishi wa umma na utendaji wa taasisi za umma,kukabiliana na ufisadi, uzembe na ubadhilifu wa mali za umma,vita dhidi ya rushwa,ujenzi wa viwanda,bandari,madini na uboreshaji wa sekta ya usafiri kwa kujenga reli ya kisasa,ununuzi wa ndege na ujenzi wa barabara.
Hata hivyo kwa upande wake Mhashamu Askofu Isaac Amani ambaye amesimikwa amesema,ni vigumu kutenganisha siasa na dini.
Ibada ya kusimikwa kwa Askofu Mkuu Isaac Amani imehudhuriwa na Maaskofu 33 wa Kanisa Katoliki,Mke wa Rais Mhe.Mama Janeth Magufuli,Waziri Mkuu Mstaafu Mhe.Mizengo Pinda,Spika Mstaafu Mhe.Anne Makinda,viongozi wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama,Wabunge,Viongozi wa Mkoa wa Arusha wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa Bw.Mrisho Gambo na wananchi wa Arusha.
Habari zaidi ni www.p5tanzania.blogspot.com

Comments

Popular posts from this blog

HISTORIA FUPI YA ABDULRAHMAN KINANA ALIYEJUZULU UKATIBU MKUU CCM

FAHAMU HISTORIA YA JOKETI ALIYETUMBULIWA NA UVCCM

HISTORIA FUPI YA LAZARO NYALANDU ALIYEIBWAGA CCM NA KUHAMIA CHADEMA