RIPOTI YA KUKAMATWA KWA WATUHUMIWA WA NYARA ZA SERIKALI KATAVI HII HAPA KUANZIA DESEMBA 24,2014--DESEMBA 30,2015


Na.Issack Gerald-Katavi
JESHI la Polisi mkoani Katavi kwa kushirikiana na askari wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA), wamefanikisha kukamata watu 11 wanaohutumiwa kumiliki nyara za serikali, yakiwemo meno ya tembo yenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 532.5 kati ya Desemba 24, 2014 na Desemba 30 mwaka 2015.
                                                              
Kamanda wa polisi Mkoani Katavi Dhahiri Kidavashari (PICHA na Issack Gerald)

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoa wa Katavi, Dhahiri Kidavashari, katika kipindi hicho vipande 67 vya meno ya tembo vyenye uzito wa kilo 155.5 vilikamatwa, vyote vikiwa na thamani ya sh milioni 515.5.
Alisema watuhumiwa saba kati ya 11 wameshafikishwa mahakamani ambapo wengine wanatumikia vifungo huku mashauri ya wengine yakiwa katika hatua mbalimbali za kusikilizwa. Watuhumiwa watatu wanaendelea kuhojiwa ambapo watafikishwa mahakamani mara tu baada ya upelelezi wa awali wa shauri lao kukamilika.
Alisema kati ya Desemba 24 mwaka 2014 na Januari 12 mwaka 2015 watuhumiwa wanne wanaosadikiwa wanamtandao wa biashara haramu ya meno ya tembo walikamatwa wakituhumiwa kukutwa na vipande 47 vya meno ya tembo vikiwa na uzito wa kilo 88.7 vyenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 306 .
Aidha, Desemba 24 mwaka 2014 saa kumi na mbili alfajiri Jeshi la Polisi mkoani humo liliwakamata watu wawili mjini Mpanda wakiwa wanataka kusafirisha vipande 22 vya meno ya tembo nyenye uzito wa kilo 46.3 vyenye thamani ya zaidi ya milioni 157 katika basi la Adventure.
Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu Kamanda Kidavashari alisema Januari 12, mwaka 2015 , saa mbili na robo usiku watuhumiwa wengine wawili walikamatwa wakiwa na vipande 25 vya meno ya tembo vikiwa na uzito wa kilo 42 vyenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 148.5.
Akifafanua, alisema watuhumiwa hao walikamatwa na askari polisi wawili waliokuwa walisindikiza basi la abiria, mali ya Kampuni ya AM yenye namba za usajili T 740 AQD lililokuwa likitokea mjini Mpanda mkoani humo na kuelekea Mwanza. “Watuhumiwa hao walikamatwa baada ya kutiliwa mashaka na askari polisi walipokuwa wakipanda basi hilo la abiria wakiwa na mabegi matatu waliyoingia nayo ndani ya gari hilo,“ alieleza.
Aprili 4 mwaka 2015, Polisi mkoani Katavi iliwakamatwa na watu wawili wakituhumiwa kukutwa na nyara ya Serikali yenye thamani ya zaidi ya Sh 49.5. Nyara hizo za Serikali zimetambuliwa kuwa ni vipande vinane vya meno ya tembo vyenye uzito wa kilo 8.2.
Alisema watuhumiwa hao walikamatwa Aprili 04, mwaka 2015 , saa sita usiku katika wakiwa katika nyumba ya kulala wageni iitwayo Salama iliyopo katika eneo la Majengo mjini Mpanda.
“Kabla ya watuhumiwa kukamatwa, Jeshi la Polisi lilipata taarifa za kiitelijensia kutoka kwa raia mwema kuwa katika nyumba ya kulala wageni ya Salama kuna wageni wawili wana meno ya tembo … mtego uliwekwa na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa,” alisisitiza.
Jeshi la Polisi mkoani Katavi liliendelea kupata mafaniko makubwa katika mapambano dhidi ya ujangili baada ya kuwakamata watu wawili wakiwa na vipande nne vya meno ya tembo vyenye uzito wa kilogramu 47.6 vyenye ya zaidi ya Sh milioni 60 .
Kwa mujibu wa Kidavashari walikamatwa Novemba 11 mwaka 2015 saa saba na nusu mchana katika kitongoji cha Tompola kijiji cha Usevya, tarafa ya Mpimbwe wilayani Mlele. Kutokana na matukio hayo, Kamanda Kidavashari ameendelea kuonya wananchi kuachana na biashara haramu za nyara za serikali na uwindaji haramu kwani ni uharibifu wa rasilimali za Taifa.

Comments

Popular posts from this blog

HISTORIA FUPI YA ABDULRAHMAN KINANA ALIYEJUZULU UKATIBU MKUU CCM

FAHAMU HISTORIA YA JOKETI ALIYETUMBULIWA NA UVCCM

HISTORIA FUPI YA LAZARO NYALANDU ALIYEIBWAGA CCM NA KUHAMIA CHADEMA