HABARI WIKI HII KUTOKA IKULU YA RAIS




1.AGIZO
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewaagiza viongozi wa Jeshi la Polisi Tanzania kuwaondoa watumishi wote wasiokuwa askari polisi na ambao wamekuwa wakijihusisha na vitendo vya ukiukwaji wa taratibu na ufujaji wa fedha za umma ili kulinda heshima, nidhamu na uadilifu ndani ya jeshi hilo.

Rais Magufuli ametoa maelekezo hayo leo tarehe 18 Julai, 2016 muda mfupi baada ya Naibu Makamishna wa Polisi 25 na Makamishna Wasaidizi Waandamizi wa Polisi 35 kula kiapo cha uadilifu kwa viongozi wa umma, Ikulu Jijini Dar es salaam.
Pamoja na kutoa agizo la kutaka wasio askari polisi kuondolewa katika utumishi wa jeshi la polisi, Rais Magufuli pia ameagiza jeshi hilo lichukue hatua dhidi ya wote wanaokabiliwa na tuhuma za wizi wa fedha wakiwemo wanaodaiwa kuiba mabilioni ya shilingi zilizotolewa kwa ajili ya ununuzi wa sare za askari mwaka jana 2015.
"Mnajua kupeleleza, mna vyombo vyote, ofisi ya IGP (Inspekta Jenerali wa Polisi) ipo palepale, ofisi ya DCI (Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai) ipo palepale, Makamishna wote mnazunguka mnakwenda palepale, mwizi mnae palepale, mnashindwa kumshika.
"Kama mnafikiri kuwa na raia katika jeshi la polisi wanawaharibia kazi zenu hamisheni raia wote na wapelekeni utumishi, kwani hakuna mhasibu ambaye ni askari polisi? hakuna mhandisi ambaye ni askari polisi? hakuna afisa tawala ambaye ni askari polisi? Mimi nafikiri kama matatizo ya wizi na wafanyakazi hewa yanaletwa na raia waliomo ndani ya jeshi la polisi na majeshi yetu mengine, IGP kaorodheshe raia wote wanafanya kazi Jeshi la Polisi ili waondolewe na tuwapangie kazi nyingine uraiani" Amesema Rais Magufuli
Hata hivyo Rais Magufuli amelipongeza Jeshi la Polisi kwa kazi nzuri linayofanya iliyoliwezesha kujenga imani kubwa kwa watanzania na ametaka viongozi wa Jeshi hilo wawaongoze askari walio chini yao vizuri, wawatie moyo na waache vitendo vya kuwakatisha tamaa kwa kuwaadhibu ama kuwatisha pale wanapochukua hatua stahiki dhidi watu wanaovunja sheria.
"Sasa mimi niwaombe nyinyi, wale wadogo mnaowaongoza mkawape mamlaka ya kutimiza wajibu wao, hata kama ameshika gari la IGP liache lishikwe IGP atakwenda kujieleza mwenyewe, hata akishika gari la RPC afanye hivyohivyo, hata akishika gari la Waziri au gari la Rais mwacheni atekeleze wajibu wake, sheria ni msumeno, tunawanyima nguvu hawa wa chini wanapotimiza wajibu wao kwa mujibu wa sheria halafu unamwambia liachie, ukifanya hivyo aliyeshikwa anatoka pale akiwa anatamba kwelikweli na yule askari unamvunja nguvu ya kufanya kazi" Amesisitiza Rais Magufuli.
Rais Magufuli pia amelitaka jeshi hilo kuungana na vyombo vingine vya serikali katika kutekeleza shughuli zake zikiwemo kusimamia ukusanyaji wa mapato ya serikali bandarini, katika sekta ya utalii na maeneo mengine, kukabiliana na vitendo vya rushwa na kuondoa watumishi hewa.
Tukio hili la Naibu Makamishna wa Polisi na Makamishna Wasaidizi Waandamizi wa Polisi kula kiapo cha uadilifu kwa viongozi wa umma limeongozwa na Kamishna wa Maadili Jaji Mstaafu Salome Kaganda na limehudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora Mhe. Anjellah Kairuki, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Hamad Yusuf Masauni, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. George Mcheche Masaju, Makatibu Wakuu na Viongozi wa vyombo vya Ulinzi na Usalama.
Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es salaam
18 Julai, 2016
………………………..
2.UTEUZI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amemteua Prof. Sylvester Michael Mpanduji kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO).
Taarifa iliyotolewa leo Ikulu Jijini Dar es salaam na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi imeeleza kuwa uteuzi wa Prof. Sylvester Michael Mpanduji umeanzia leo tarehe 18 Julai, 2016.
Kabla ya uteuzi huu Prof. Sylvester Michael Mpanduji alikuwa Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA).
Prof. Sylvester Michael Mpanduji anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Mhandisi Omary Jumanne Bakari ambaye uteuzi wake umetenguliwa.
Wakati huo huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amemteua Dkt.Winnie Mpanju-Shumbusho kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Benjamini Mkapa - Dodoma.
Kabla ya Uteuzi huo, Dkt. Winnie Mpanju-Shumbusho alikuwa Mkurugenzi Mkuu Msaidizi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) lenye makao yake makuu Mjini Geneva nchini Uswisi na alimaliza mkataba wake tangu Mwezi Desemba 2015.
Uteuzi wa Dkt. Winnie Mpanju-Shumbusho umeanza leo tarehe 18 Julai, 2016.
Dkt. Winnie Mpanju-Shumbusho anachukua nafasi iliyoachwa wazi na Dkt. Donan William Mmbando ambaye ameomba kupumzika kutokana na sababu binafsi.
Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es salaam
18 Julai, 2016 
………………………..
3.MIKOPO
Benki ya Exim ya China imekubali kutoa mkopo wenye masharti nafuu wa dola za Marekani Bilioni 7.6  sawa na zaidi ya Shilingi Trilioni 16 za kitanzania kwa ajili ya kugharamia ujenzi wa mradi mkubwa wa reli ya kati hapa nchini kwa kiwango cha kisasa (Standard Gauge) unaotarajiwa kuanza katika mwaka huu wa fedha.
Rais wa Benki ya Exim ya China Bw. Liu Liang amemueleza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 20 Julai, 2016 katika Ikulu ndogo ya Chamwino Mkoani Dodoma kuwa pamoja na kutoa fedha hizo zitakazofanikisha ujenzi wa kilometa 2,190 za reli ya kati benki hiyo itashirikiana na Tanzania  katika kubadilishana uzoefu na utaalamu katika ujenzi na uendeshaji wa reli.
Pamoja na kukubali kutoa fedha hizo, Rais huyo wa Benki ya Exim ya China amempongeza Rais Magufuli na serikali yake kwa dhamira ya dhati ya kuiletea nchi maendeleo ikiwemo kuharakisha ujenzi wa reli ya kati na ameahidi kuwa benki yake itatoa ushirikiano wa karibu katika kufanikisha mradi huo na miradi mingine ya maendeleo.
"Kuhusu huu mradi wa reli ya kati tuna mtazamo chanya, tunauona ni mradi mzuri na tutatoa ushirikiano wowote utakaohitajika. Tunaamini kuwa kwa ushirikiano na serikali ya Tanzania mchakato wa utekelezaji wa mradi huu utafanyika kwa mafanikio na kwa kuzingatia muda" Amesema Rais Magufuli.
Kwa upande wake Rais Magufuli amemshukuru Rais wa Benki ya Exim ya China Bw. Liu Liang kwa kukubali kutoa fedha hizo na amemuhakikishia kuwa Tanzania imedhamiria kutekeleza mradi huo ambao tayari ujenzi wake umepangwa kuanza katika mwaka huu wa fedha kwa kutumia fedha za ndani kiasi cha shilingi Trilioni 1 zilizotengwa katika bajeti.
Rais Magufuli amebainisha kuwa kutekelezwa kwa mradi huo kutasaidia kuinua uchumi wa Tanzania na nchi jirani zisizopakana na bahari zikiwemo Uganda, Rwanda, Burundi, na Congo.
"Kwa hiyo kukubali kwao ambako ilikuwa ni kitu kikubwa, inaonesha kwamba juhudi za Tanzania kwenda haraka haraka zinakubalika kimataifa, na wenzetu hawa wachina wana pesa nyingi.
"Na kule kuaminika kwamba tunakopeshwa kwa masharti nafuu, riba yake ni ndogo na huku kwetu ni mafanikio makubwa, kwa hiyo mizigo mingi tutakuwa tunaisafirisha, tutaendeleza reli yetu na bandari zetu" Amesema Rais Magufuli.
Mradi wa ujenzi wa reli ya kati utahusisha ujenzi wa reli kwa kiwango cha kisasa (Standard Gauge) kutoka Dar es salaam-Tabora-Isaka-Mwanza, Tabora-Mpanda-Kalemela, Tabora-Uvinza-Kigoma na Isaka-Keza-Msongati.
Mazungumzo kati ya Rais Magufuli na Rais wa benki ya Exim ya China yamehudhuriwa na Balozi wa China hapa nchini Dkt. Lu Youqing, Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa Mnyaa, Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Suzan Kolimba.
Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dodoma
20 Julai, 2016

Comments

Popular posts from this blog

HISTORIA FUPI YA ABDULRAHMAN KINANA ALIYEJUZULU UKATIBU MKUU CCM

FAHAMU HISTORIA YA JOKETI ALIYETUMBULIWA NA UVCCM

HISTORIA FUPI YA LAZARO NYALANDU ALIYEIBWAGA CCM NA KUHAMIA CHADEMA